Tanzania Anthem

Monday, 16 June 2014

PATA HABARI NZIMA YA DODOMA FM YA LEO HAPA



DODOMA
Wananchi pamoja na viongozi mbalimbali Mkoani Dodoma wametakiwa kutambua umuhimu wa kuchangia damu  salama ili kuweza kuokoa maisha ya  wagonjwa wengine.
Wito huo umetolewa na Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Dr.Zainabu Chaula katika maadhimisho ya uchangiaji Damu yaliyofanyika mwishoni mwa wiki ambapo amesema kuwa kumekuwa na vifo vingi vya akina mama wajawazito wakati wa kujifungua hivyo ni  vyema wananchi wajitokeze kuchangia damu.

Nae Mkuu wa Kitengo cha damu Salama Mkoani Dodoma Dr.Lea Kitundya amesema siku ya maadhimisho ya uchangiaji wa damu salama duniani ni siku ya kuwaenzi wale wote wanaojitolea katika suala zima la kuchangia damu .
Aidha Dr.Lea amewataka  wananchi waendelee kujitokeza  kwa wingi katika  uchangiaji damu  salama kwani  kuna uhaba mkubwa wa ukosefu wa damu .
Kwa upande wa wachangiaji damu waliohudhuria katika hafla hiyo  wamesema wameipokea vizuri siku ya maadhimisho hayo kwani inasaidia kupunguza tatizo la watu wanaopoteza maisha yao kutokana na upungufu wa damu na kuwataka watu wengine wahamasike ili kuweza kuokoa maisha ya watanzania wengine.
Serikali kupitia wizara ya  afya  imeanzisha  ujenzi wa Hospitali itakayo kuwa na uwezo wa kutoa huduma zisizo patikana  hapa nchini.
Hayo yamesemwa na Naibu waziri  Tamisemi Bw. Agrey Mwanri alipokuwa akijibu  swali lililoulizwa na Mbunge wa Viti Maalumu Elizabeth Batenga alietaka kujua mwongozo wa wizara ya afya juu ya kulinda afya za wananchi bila kujali hali zao kichumi .  
Aidha Waziri Mwanri amesema  kuwa upo mfumo wa rufaa kwa wagonjwa wote kuanzia ngazi ya Zahanati hadi  Hospitali ya Taifa  kwenda kutibiwa Nje ya Nchi kwa gharama za Serikali.
Pia amesema Serikali ina mfumo wa kutoa matibabu bure kwa  wagonjwa mbalimbali ikiwemo mama mjamzito na  wagonjwa wenye magonjwa sugu kama saratani,kifua kikuu,kisukari,ukimwi , magonjwa ya akili, pamoja na wazee wa umri zaidi ya miaka sitini.
Serikali imeeleza kuwa Tanzania haina budi kuhakikisha inajenga  uchumi wenye misingi imara  na uwezo wa ushindani utakaowezesha kukabiliana na changamoto za maendeleo.
Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa kamati ya bajeti Bwana Andrew Chenge alipokuwa akitoa taarifa ya kamati ya bajeti bungeni ambapo amesema Tanzania ni lazima ijenge misingi imara ya uchumi wenye ushindani.
Aidha Bwana Chenge amebainisha kuwa takwimu za mwenendo wa ukuaji wa uchumi nchini kwa miaka mitatu mfululizo ni wa kuridhisha na umekuwa kwa wastani wa asilimia 6.8
Kwa upande wake msemaji wa kambi rasmi bungeni kwa upande wa wizara ya mahusiano na uratibu Bi Ester Matiku  amesema ni vyema viongozi kuondoa umaskini unao wakabili watanzania bila kujali itikadi za vyama vyao.
KITAIFA
Jeshi la Polisi Zanzibar limesema bomu la kurushwa lililolipuka  katika eneo la Darajani na kusababisha kifo cha mtu mmoja na kujeruhi wengine saba ni la kivita lililotengenezwa kiwandani.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi, Mkadam Khamis amesema kwamba uchunguzi wa awali umebaini bomu hilo hutumika kwa shughuli za kivita na kwamba hiyo ni mara ya pili kwa bomu kama hilo kutumika katika matukio tofauti Zanzibar.
Hata hivyo, Kamanda Mkadam amesema hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa kuhusiana na tukio hilo na uchunguzi unaendelea ili kuwabaini wahusika na kupitia mikanda ya video na kusikiliza mawaidha yaliyokuwa yakitolewa na Sheikh Kassim ili kuwasaidia kubaini chanzo.
Bomu hilo lilirushwa na kulipuka muda mfupi baada ya watu kuhudhuria mawaidha msikitini yaliyokuwa yakitolewa na Sheikh Kassim Mafuta  kutoka Tanga ambaye kutokana na tukio hilo, amesitisha ziara yake Zanzibar kwa sababu za kiusalama.
KIMATAIFA
Shirika la uhamiaji la kimataifa limesema linahitaji dola milioni 97.2 za kimarekani ili liendelee kutoa misaada ya kibinadamu nchini Sudan Kusini hadi mwezi Desemba.
Shirika hilo limebadilisha makadirio ya fedha linazohitaji kutokana na hali halisi nchini Sudan Kusini ambapo zaidi ya watu milioni moja waliokimbia makazi yao wanahitaji msaada wa kibinadamu.
Kwa mujibu wa Shirika la uhamiaji la kimataifa zaidi ya watu elfu 94 wanahifadhiwa katika sehemu zinazowahifadhi watu wanaohitaji ulinzi.
Watu wanaoshukiwa kuwa wapiganaji wa Kiislamu wameshambulia kituo cha polisi, mahoteli na vijiji mbalimbali mjini Mpeketoni  pwani ya Kenya .
Shambulizi lilifanyika usiku wa june 15 ambapo  watu waliokuwa wamejifunika nyuso zao wakiwa wamejihami vikali walivamia vituo  vya polisi ,hoteli na benki.
Duru kutoka kisiwa cha Lamu zimearifu kuwa wapiganaji hao walifika katika malori mawili na kurusha kifaa kama bomu ndani ya kituo cha polisi kisha wakavamia na kuiba silaha.
Baadhi ya walioshuhudia wamearifu  kuwa wameona maiti kadhaa na majeruhi wengi japo Polisi hawajathibitisha ni watu wangapi wameuawa.
Shirika la msalaba mwekundu linasema kuwa hadi kufikia sasa watu 48 wanahofiwa kuuawa katika shambulizi hilo lililotokea  June 15 mwaka huu.
Mkuu wa tume ya Umoja wa Mataifa ya kuleta utulivu nchini Mali Bw Albert Koenders  amesema mchakato wa mapatano nchini Mali unapaswa kuhusisha watu wote ili kufikia amani ya kudumu.
Bw Koenders amefafanua kuwa mgogoro wa Mali unapaswa kujadiliwa na mazungumzo ya amani yaliyoongozwa na Algeria hivi karibuni kati ya serikali ya Mali na waasi na kusema ni muhimu na ni ya kipaumbele katika kusukuma mbele majadiliano jumuishi.
Maofisa wa Umoja wa Mataifa wameipongeza Algeria kwa kazi yake ya kiujenzi katika kuanzisha amani na maelewano nchini Mali, na kusema ukanda wa Sahel upo hatarini kama hakutakuwa na amani na usalama nchini Mali.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Blog Archive